“Hawa Wadhihirishaji watakatifu wamekuwa kama ujio wa kipindi cha majira ya machipuko ulimwenguni…kwa kuwa majira ya machipuko ni wakati wa uumbaji mpya….”— ‘Abdu’l‑Bahá

Imani ya Kibahá’í ilianza na utume ambao Mungu aliwakabidhi Mitume Watakatifu wawili—Báb na Baháu’lláh. Leo, umoja wa kipekee wa Imani Waliyoianzisha hutokea kutoka maagizo ya wazi yaliyotolewa na Bahá’ú’lláh ambayo yamehakikishia mwongozo endelevu baada ya kupaa Kwake. Mlolongo huu wa urithi, ujulikanao kama Agano, ulitoka kwa Bahá’u’lláh hadi kwa Mwanaye ‘Abdu’l-Bahá, na halafu kutoka kwa ‘Abdu’l-Bahá hadi kwa mjukuu Wake, Shoghi Effendi, na Nyumba ya Haki ya Ulimwengu, iliyoamriwa na Bahá’u’lláh. Mbahá’í anakubali mamlaka takatifu ya Báb na Bahá’u’lláh na warithi hawa walioteuliwa.

Báb »

(1819-1850)

Báb ni Mtangulizi wa Imani ya Kibahá’í. Katikati ya karne ya 19, Alitangaza kwamba Yeye alikuwa mchukuzi wa ujumbe uliokusudiwa kubadilisha maisha ya kiroho ya binadamu. Utume Wake ulikuwa ni kuandaa njia kwa ajili ya ujio wa Mtume wa pili kutoka kwa Mungu, mkuu kuliko Yeye Mwenyewe, ambaye angeleta zama ya amani na haki.

Bahá'u'lláh »

(1817-1892)

Bahá’u’lláh—“Utukufu wa Mungu”—ni Yule Mwahidiwa aliyetabiriwa na Báb na Mitume wote wa Mungu wa wakati uliopita. Bahá’u’lláh aliwasilisha Ufunuo mpya kwa binadamu kutoka kwa Mungu. Maelfu ya aya, barua na vitabu vilitiririka kutoka kalamu Yake. Katika Maandiko Yake, Alichora mfumo kwa ajili ya maendeleo ya ustaarabu wa ulimwengu, ambao unazingatia vyote viwili vipengele vya kiroho na vya kimwili vya maisha ya binadamu. Kwa hili, Alivumilia miaka 40 ya kifungo, mateso na uhamisho.

‘Abdu’l‑Bahá »

(1844-1921)

Katika wasia Wake, Bahá’u’lláh alimteua mwanawe wa kwanza, ‘Abdu’l-Bahá, kama mfasiri mwenye mamlaka wa mafundisho Yake na Mkuu wa Imani. Kote Mashariki na Magharibi, ‘Abdu’l-Bahá alipata kujulikana kama balozi wa amani, mfano wa mwanadamu anayestahili sifa, na mtetezi mashuhuri wa Imani mpya.

Shoghi Effendi »

(1897-1957)

Aliyeteuliwa kuwa Mlezi wa Imani ya Kibahá’í na ‘Abdu’l-Bahá, mjukuu Wake wa kwanza, Shoghi Effendi, alitumia miaka 36 kulea kiutaratibu maendeleo, kukuza uelewa, na kuimarisha umoja wa jumuiya ya Kibahá’í, wakati ilipoendelea kukua na kuakisi anuwai ya mbari nzima ya binadamu.

Nyumba ya Haki ya Ulimwengu »

(established 1963)

Maendeleo ya Imani ya Kibahá’í kote ulimwenguni leo huongozwa na Nyumba ya Haki ya Ulimwengu. Katika Kitabu Chake cha Sheria, Bahá’u’lláh aliiagiza Nyumba ya Haki ya Ulimwengu kutumia athari chanya juu ya hali njema ya binadamu, kuendeleza elimu, amani na ustawi wa wote, na kuhifadhi heshima ya kibinadamu na wadhifa ya dini.