“Msingi ambao juu yake utaratibu huu wa kiutawala umewekwa ni Kusudi lisilobadilika la Mungu kwa binadamu katika siku hii. Chanzo ambacho kutoka kwake unapata upuzio wake siyo kingine ila Bahá’u’lláh Mwenyewe.” –Shoghi Effendi

Utaratibu wa Kiutawala wa Kibahá’í

Shughuli za jamii ya Kibahá’í hutawaliwa kupitia mfumo wa asasi, kila moja na uwanja wa utendaji uliowekwa dhahiri. Machimbuko ya mfumo huu—unaojulikana kama Utaratibu wa Utawala wa KiBahá’í—hupatikana katika Maandiko ya Bahá’u’lláh Mwenyewe. Alifunua kanuni zinazoongoza utendaji wake, kuanzisha asasi zake, kumteua ‘Abdu’l-Bahá kama mfafanuzi pekee wa Neno Lake, na kujalia mamlaka kwa Nyumba ya Haki ya Ulimwengu. Katika Wasia Wake na Agano , ‘Adu’l-Baha alimteua mjukuu wake Shoghi Effendi, kama Mlezi wa Imani ya Kibahá’í. Kuanzia mwanzo wa uchungaji wake, Shoghi Effendi aliweka wakfu juhudi kwa maendeleo ya Utaratibu wa Kiutawala, akiuleta katika uwepo katika umbo lake la kiinitete (mwanzo) na kuandaa njia kwa uchaguzi wa Nyumba ya Haki ya Ulimwengu.

Leo Nyumba ya Haki ya Ulimwengu ni chombo kikuu cha utawala cha Utaratibu wa Kiutawala. Chini ya mwongozo wake, mabaraza yanayochaguliwa, ambayo hujulikana kwa jina Mabaraza ya Kiroho ya Mahali na Mabaraza ya Kiroho ya Taifa yanachunga shughuli za jumuiya ya Kibahá’í kwenye ngazi yao husika, yakitekeleza mamlaka ya utungaji sheria, ya utendaji, na ya kimahakama. Asasi ya watu wenye uwezo uliothibitishwa wanaoteuliwa—asasi ya Washauri—pia hufanya kazi chini ya mwongozo wa Nyumba ya Haki ya Ulimwengu na hutoa nguvu yenye ushawishi katika ya Maisha ya jumuiya ya Kibahá’í, kuanzia mashinani hadi ngazi ya kimataifa. Wajumbe wa Asasi hii wanahimiza utendaji, kulea ari ya mtu binafsi, na kukuza ujifunzaji katika jumuiya ya Kibahá’í kwa ujumla, pamoja na kutoa ushauri kwa Mabaraza ya Kiroho.

Zikifanya kazi katika dhima zao husika, asasi za Washauri na Mabaraza ya Kiroho vinashiriki madaraka kwa ajili ya ulinzi na uenezaji wa Imani ya Kibahá’í. Mwingiliano patanishi kati yao huhakikishia utoaji endelevu wa mwongozo, upendo, na uhamasishaji kwa wajumbe wa jumuiya ya Kibahá’í kote ulimwenguni. Kwa pamoja, wanachangamsha jitihada za watu binafsi na za pamoja kuchangia kwenye ustawi wa jamii.

Asasi za Kibahá’í hazifikiriwi tu kama nyenzo ya kutawala vipengele vya ndani vya maisha ya jumuiya ya Kibahá’í, ingawaje hii ni ya muhimu. Kwanza, Utaratibu wa Kiutawala umekusudiwa kufanya kazi kama njia ambayo kupitia kwake roho ya Imani hutiririka, ikijumuisha katika utendaji wake aina ya mahusiano ambayo lazima yaje kuunganisha na kudumisha jamii kadri ambavyo wanadamu huelekea kwenye ukomavu wa pamoja.


“Ni muundo wa Utaratibu Mpya wa Kiulimwengu, unaoamka sasa katika tumbo la uzazi la asasi za kiutawala ambazo Yeye Mwenyewe ameziunda, ambazo zitatumika kama yote mawili mkondo na kiini cha ile jumuiya ya kiulimwengu ambayo ni hatima ya hakika, na kusudio lisiloepukika la watu na mataifa ya dunia.”

— Shoghi Effendi

{{ note }}: